KIVAZI cha ndugu wa maharusi, kimesababisha patashika katika Kanisa
Katoliki, Parokia ya Mtakatifu Peter, baada ya Paroko Msaidizi wa Kanisa
hilo, Padri Paulo Haule, kusitisha ibada mpaka mhusika atoke akavae
vizuri.
“Ninatoa dakika 10 kwa aliyeingia na mavazi ambayo hayatakiwi
kanisani humu kutoka mara moja akavae vizuri, la sivyo ndoa yao
haitafungwa,” alisema Padri Haule wa Kanisa hilo lililoko Oysterbay, Dar
es Salaam.
Awali vurugu hizo zilizotokea Jumamosi iliyopita, zilianzia nje,
wakati Katekista wa Parokia hiyo, Yohane Maboko, alipotangazia wanandoa
na ndugu zao waliokuwa mabega wazi au kuvaa nguo fupi, kutafuta nguo za
kujifunika au wasiingie kabisa kanisani.
Maharusi walikubali kutekeleza ombi hilo, wakavishwa vitambaa
mabegani vya rangi tofauti na gauni jeupe la harusi, wakaruhusiwa
kuingia kanisani, tayari kufunga pingu zao za maisha.
Hata hivyo, mmoja wa ndugu wa maharusi hao ambaye jina lake
halikupatikana mara moja, alipotaka kulazimisha kuingia na kivazi chake
cha mabega wazi, alizuiwa na Katekista Maboko. Katekista huyo alimfuata
mwanamke huyo ili kumrudisha akavae vizuri, lakini aliibua zogo na
kulazimisha kuingia na vazi hilo.
Zogo hilo lilipoendelea, wanandugu waliingilia kati, wakitetea vazi
hilo ambapo mmoja wa wanandugu, alimvua miwani Katekista Maboko na
kuipiga chini ikavunjika huku yeye na wenzake wakimtolea maneno makali
ya kumtaka asimzuie ndugu yao kuingia kanisani.
Wakati ndugu hao
wakimdhibiti Katekista Maboko, mwanamke huyo alitumia mwanya huo na
kupenya hadi ndani ya Kanisa, ambamo Padri Haule, alikuwa akijiandaa
kuanza ibada.
Baada ya Padri Haule kupata taarifa, alitangaza
kuwa ndoa ya maharusi wa msichana huyo, haitafungwa hadi awe ametoka.
Licha ya Paroko kutangaza hivyo, bado ukaidi uliendelea jambo
lililomfanya Katekista Maboko kumfuata tena dada huyo na kumwamuru atoke
nje, ambapo aliendelea kupinga na baadaye akatekeleza amri hiyo ya
Paroko.
Baada ya hapo shughuli za kufungisha ndoa ziliendelea kwa amani
na utulivu hadi mwisho maharusi wakatoka kwenda kuendelea na mambo
mengine.
Akizungumza na mwandishi wetu, Katekista Maboko alisema waumini hao
walikiuka maadili ambayo Kanisa lina wajibu wa kulinda na kuyasimamia
ili waumini wake wayafuate.
Alisema miwani yake iliyovunjwa ilikuwa na
thamani ya Sh 90,000 na baada ya ibada hiyo, aliyetenda kosa hilo
alimwendea na kumwomba radhi na kulipa Sh 50,000 na kuahidi kumalizia
kiasi kilichobaki wakati wowote.
Maboko alisema uvaaji wa mavazi yasiyotakiwa kanisani hapo, umekuwa
ukipigiwa kelele mara kwa mara, na hata katika mafundisho ya ndoa
huambiwa lakini ukaidi unaendelea.
“Maharusi wakati wa mafundisho ya ndoa tunawaambia kuhusu mavazi yao na hata ya ndugu zao watakaowasindikiza kanisani, kuwa wavae kistaarabu lakini hawasikii,” alisema Katekista Maboko.
Makanisa mengi siku hizi yamekuwa yakipiga marufuku uvaaji wa nguo fupi na zinazoacha mabega wazi kwa wasichana na wanawake, wakati wa ibada za kawaida na za ndoa.
Habarileo
0 comments:
Post a Comment